Thursday, December 19, 2013

Elimu

Kukosa kuungwa mkono na wazazi, walezi pamoja na kuamini kuwa kunahitajika nguvu kubwa katika utendaji wa kazi imedaiwa kuwa chanzo cha wasichana kukimbia masomo ya sayansi na uhandisi.

Hayo yalisemwa na baadhi ya washiriki wa mafunzo ya mafundi wa majokofu na viyoyozi kuhusu teknolojia mbadala za upozaji rafiki kwa tabaka la Ozoni yanayofanyika katika Hoteli ya Paradise Jijini Mbeya.

Mkufunzi kutoka Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia (Must), Moses Malole alisema kuwa imani kuwa kazi za uhandisi zinahitaji matumizi ya nguvu pamoja na kutoungwa mkono na wazazi imekuwa ni kichochea cha idadi kubwa ya wasichana kuyaepuka masomo ya uhandisi na sayansi.

Akitoa mfano alisema kati ya wasichana wanne waliokuwa wanasoma masomo ya kozi ya awali ya uhandisi (Bridging course) kabla ya kuungana na waliosoma diploma, wanafunzi watatu walijitoa katika kozi hiyo na kuhamia katika kozi nyingine kwa kuhofia ugumu wa masomo.

Hata hivyo alisema kazi nyingi za uhandisi ikiwemo ufundi wa majokofu hazitumii nguvu na kwamba kinachohitajika hivi ni kuongezeka kwa juhudi za kuwahamasisha wasichana waweze kushiriki katika masomo ya sayansi na uhandisi kwa kuwa ni rahisi na pia yanamanufaa katika jamii.

Kwa upande wake, Mkurugenzi msaidizi idara ya mazingira kutoka ofisi ya Makamu wa Rais, Magdalena Mtenga alisema kuwa serikali imeanza kuchukua juhudi za makusudi katika kuwahamasisha wasichana ili waweze kushiriki katika masomo ya sayansi badala ya kuwa fani ya wanaume pekee.

Alisema baadhi ya juhudi imekuwa ni pamoja na kuwasomesha ambapo hata hivyo alisema juhudi za pamoja kati ya serikali na wananchi zinahitajika ili kuweza idadi kubwa ya wasichana kujiunga na masomo ya sayansi.

Aidha alisemawazazi na walezi wanatakiwa waunge mkono kwa kuwahamasisha wasichana na si kuwakatisha tamaa kwa kuwaambia ni masomo magumu na hawayawezi.

Warsha ya mafunzo ya mafundi wa majokofu na viyoyozi inahusisha washiriki kutoka Mikoa ya Mtwara, Lindi, Mbeya, Rukwa, Katavi, Ruvuma na Iringa hata hivyo kati ya washiriki wote hakuna mshiriki wa kike hata mmoja.

No comments:

Post a Comment