Wednesday, December 18, 2013

Kilimo

Wakulima wilayani Chunya wameingiza shilingi bilioni 90 katika msimu wa kilimo uliopita kutokana na mauzo ya mazao ya ufuta,karanga, alizeti na tumbaku.
Mkuu wa wilaya ya Chunya, Deodatus Kinawilo aliyasema hayo alipokuwa akizungumza wakati wa ufungaji wa mafunzo ya kuvijengea uwezo vikundi vya wakulima wa zao la alizeti wilayani humo.
Alisema kuwa kutokana na mapato hayo inadhihirisha kuwa shughuli za kilimo zinamanyfaa kiuchumi kutokana na wakulima kuweza kupata shilingi bilioni tisini katika msimu mmoja wa kilimo ambapo alisema kuwa wananchi wanatakiwa kuacha kulalamikia ugumu wa maisha na badala yake wafanye kazi.
Akitoa mchanganuo wa mapato hayo, Kinawilo alisema wakulima wa alizeti walipata shilingi bilioni nne, ufuta bilioni 27, karanga bilioni 12 na tumbaku bilioni 47, hata hivyo alisema licha ya mapato hayo eneo linalolimwa ni dogo ikilinganishwa na eneo linalofaa kwa kilimo.
Alisema eneo linalofaa kwa kilimo wilayani Chunya ni kilomita za mraba 19,800 sawa na asilimia 66 na kwamba kati ya eneo hilo, eneo linalotumika kwa kilimo ni kilomita za mraba 2,276 sawa na asilimia saba ambapo alisema mkulima akijitahidi sana analima ekari mbili tu.
Aidha alisema mkulima wilayani humo akifuata kanuni bora za kilimo anaweza kuvuna gunia 25 za kilo 60 kila moja kwa ekari, lakini hivi sasa wanavuna kati ya gunia 4-12 kwa ekari.
Awali, Mkurugenzi wa Taasisi ya watetezi wa mazingira na kilimo endelevu (KAEA), Lucas Malangalila alisema katika utafiti wa awali walibaini kuwa kilimo cha zao la alizeti kinakabiliwa na changamoto nyigi ikiwamo ukosefu wa soko la uhakika na uzalishaji mdogo wa wakulima, mbegu zilizo chini ya kiwango pamoja na kukosekana kwa dhamira ya dhati ya wananchi kuondokana na umasikini kupitia zao hilo.
Alisema baada ya kutambua changamoto zinazowakabili wakulima, walivitambua vikundi vya wakulima na kuwapa mafunzo ya mwenendo wa uongozi, masuala ya jinsia na kilimo cha mikataba na kuwakutanisha na wanunuzi na wasindikaji.

No comments:

Post a Comment